Main Body

Onyesho la Pili: Muhtasari

Wanawake wanashindwa kuinua Nguzo Mama. Inawabidi kukaa pamoja ili kujadiliana nini wafanye. Bi. Nane anapendekeza waivute Nguzo Mama kwa kamba lakini Bi. Nne anapinga wazo hilo. Baada ya mazungumzo marefu, wanakubaliana kwamba wafanye miradi itakayowaletea pesa kwa haraka. Wakiwa na pesa, Nguzo Mama itasimama maana ‘Pesa msema kweli.’ Bi. Pili anaamua kutengeneza pombe ya kuuza ili apate pesa. Hata hivyo, anashindwa kufanikiwa kwa sababu ya mume wake kuchukua pesa anazopata kwa kuuza pombe. Wanawake wengine wanaanza biashara ya kutengeneza na kuuza vitambaa. Mara ya kwanza vitambaa vinanunuliwa sana na kweli wanapata pesa. Lakini baadaye kila mji unakuwa na vitambaa, wengine wanajifunza kushona na hivyo wanajishonea vitambaa vyao wenyewe. Hakuna haja ya kununua vitambaa tena. Biashara ya vitambaa inakwama kwa sababu ya kukosa soko (wanunuzi). Lakini pia wanawake wenyewe wanachukiana. Bi. Nne, ambaye ni kiongozi wa wanawake hampendi Bi. Nane ambaye ni mwalimu. Hali hii inasababisha wao kushindwa kufanya kazi pamoja. Bi. Nne anamshtaki Bi. Nane kwa mwenyekiti wa Kamati ya Mashauri ya mji. Bi. Nane anatuhumiwa kwa kuunda kikundi cha kupinga juhudi za kina mama wengine za kusimamisha Nguzo Mama. Madai haya anayakataa kuwa ni uongo. Hata hivyo, Bi. Nane anakataa kusema maelezo yake kwa mdomo. Anasema atatoa maelezo yake kwa maandishi. Wakati haya yote yanaendelea, Nguzo Mama bado imelela chini.

License

Materials for Swahili Learners Copyright © by kdthomp3. All Rights Reserved.